![]() |
| Baba wa Taifa Mwalimu J.K Nyerere |
Mwalimu alikuwa rais wa kwanza wa Tanzania, Alizaliwa katika kijiji cha Butiama, mkoani Mara pembezoni mwa Ziwa Nyanza (sasa Victoria) tarehe 13 Aprili, 1922. Alifariki dunia tarehe 14 Oktoba, 1999.
Aliiongoza Tanzania toka mwaka 1961 hadi mwaka 1985.
Yeye ni mwasisi wa itikadi ya UJAMAA na KUJITEGEMEA na Kabla ya kuingia kwenye siasa alikuwa ni mwalimu, Kazi hii ndiyo ilimpatia jina ambalo lilimkaa maisha yake yote la "Mwalimu."
Mwalimu Nyerere ni kati ya viongozi wachache wa Afrika ambao wameacha madaraka kwa hiyari baada ya kutawala kwa muda mrefu. Alipostaafu urais mwaka 1985 alirudi kijijini kwake Butiama ambako aliendesha shughuli za kilimo. Aliendelea kuwa na ushawishi mkubwa katika siasa ya Tanzania hadi kifo chake.
Julius Kambarage Nyerere alizaliwa mwaka 1922 ( katika kijiji cha Butiama, wilaya ya Musoma, mkoa wa Mara, Tanzania (wakati ule: Tanganyika). Alikuwa mmojawapo kati ya watoto 26 wa Nyerere Burito, chifu wa kabila la Wazanaki.
Alipokuwa mtoto Nyerere alichunga mifugo ya baba yake; katika umri wa miaka 12 aliingia shule akitembea kilomita 30 hadi Musoma. Baada ya kumaliza shule ya msingi aliendelea kusoma shule ya wamisionari Wakatoliki huko Tabora. Katika umri wa miaka 20 alibatizwa akawa mkristo Mkatoliki hadi mwisho wa maisha yake.
Mapadre wakatambua juhudi zake katika elimu wakamsaidia kusoma ualimu huko chuo kikuu cha Makerere, Kampala, Uganda kuanzia 1943 - 1945.Julius Nyerere alipokuwa Makerere akaanzisha tawi la Umoja wa wanafunzi Watanganyika pia alijihusisha na uundwaji wa tawi la Tanganyika African Association (TAA). Baada ya kumaliza masomo ya ualimu alirudi Tabora akafundisha shule ya St.Mary´s.
Mwaka 1949 alipata ufadhili (Scholarship) kwenda kusoma Chuo Kikuu cha Edinburgh huko Uskoti Uingereza akasoma shahada ya uzamili katika historia na uchumi. Alikuwa mtanzania wa kwanza kusoma katika chuo kikuu nchini Uingereza na mtanzania wa pili kupata shahada ya elimu ya juu nje ya Tanzania.
![]() |
| Mwalimu Nyerere katika moja ya hotuba zake |
Aliporejea Tanganyika kutoka masomoni, Nyerere alifundisha Historia, Kingereza na Kiswahili katika shule ya St. Francis iliyo karibu na Dar es Salaam. Mwaka 1953 alichaguliwa kuwa raisi wa chama cha Tanganyika African Association (TAA), chama ambacho alikisaidia kukijenga alipokuwa mwanafunzi katika chuo kikuu cha Makerere. Mwaka 1954 alikibadilisha chama cha TAA kwenda katika chama cha Tanganyika African National Union (TANU) ambacho kilikuwa cha kisiasa zaidi kuliko TAA. Ndani ya mwaka mmoja chama cha TANU kilikuwa tayari ni chama kikuu cha siasa kinachoongoza Tanganyika.
Uwezo wa mwl. Nyerere uliwashitua uongozi wa kikoloni na kumlazimisha Nyerere kuchagua kati ya siasa na kazi ya ualimu.
Nyerere alisikika akisema kuwa alikuwa mwalimu kwa kuchagua na mwanasiasa kwa bahati mbaya. Alijiuzuru ualimu na kuzunguka nchini Tanganyika kuzungumza na watu wa kawaida na machifu ili kuleta muungano katika kupigania uhuru.
Mwalimu Pia alizungumza kwa niaba ya TANU katika Trusteeship council na Fourth committee ya Umoja wa Mataifa (UN) huko New York. Uwezo wake wa kidiplomasia na kuunganisha watu ulimwezesha kufanikisha Tanganyika kupata uhuru bila kumwaga damu.
Ushirikiano mzuri aliouonyesha aliyekuwa gavana wa wakati huo bwana Richard Turnbull ulisaidia pia kuharakisha upatikanaji wa uhuru.
Nyerere aliingia katika bunge la kikoloni mwaka 1958 na kuchaguliwa kuwa waziri mkuu mwaka 1960. Mwaka 1961 Tanganyika ilipata uhuru wake na tarehe 9/12/1961 Nyerere alichaguliwa kuwa waziri mkuu wa Tanganyika huru na mwaka mmoja baadae Nyerere alikuwa raisi wa kwanza wa jamhuri ya Tanganyika.
Nyerere alikuwa kiungo muhimu katika muungano wa Tanganyika na Zanzibar kutengeneza Tanzania baada ya mapinduzi ya Zanzibar mwaka 1964 yaliyomtoa madarakani sultani wa Zanzibar Jamshid bin Abdullah.
| Nyerere akichanganya ardhi ya Zanzibar na Tanganyika wakati wa muungano 1964 |
Tarehe 5 Februari 1977 aliongoza chama cha TANU katika kuungana na chama tawala cha Zanzibar ASP (Afro-shiraz Party) na kuanzisha chama kipya cha CCM (Chama cha Mapinduzi) akiwa mwenyekiti wake.
Nyerere aliendelea kuongoza Taifa hadi 1985 alipomwachia nafasi raisi wa awamu ya pili Ali Hassan Mwinyi.
Mwalimu Aliendelea kuongoza Chama cha Mapinduzi hadi mwaka 1990 na kuwa ushawishi mkubwa katika siasa ya Tanzania hadi kifo chake.
Inasadikika kuwa Nyerere alishawishi uteuzi wa Benjamini W. Mkapa kama mgombea wa urais katika uchaguzi mwaka 1995, na ambaye ndiye aliyechaguliwa kuwa rais katika uchaguzi huo.
Nyerere alikaa muda mwingi nyumbani kwake Butiama akijihusisha na kilimo. Pamoja na haya alianzisha taasisi yenye jina lake; mwaka 1996 alikuwa mpatanishi wa pande zinazokinza, katika vita ya wenyewe kwa wenyewe huko Burundi.
Tarehe14 oktoba .1999 alifariki dunia katika hospitali ya Mtakatifu Thomas mjini London Uingereza, baada ya kusumbuliwa na tatizo la saratani ya damu (leukemia) , iliyosababisha mauti yake.
MAFANIKIO YAKE
- kujenga umoja wa Taifa na utamaduni wa Kiafrika pamoja na lugha ya Kiswahili,
- kushinda ubaguzi wa rangi, na juhudi zake kuchangia Taifa la Afrika kusini huru.
- kutetea usalama wa taifa katika vita vya kagera dhidi ya Nduli Iddi Amin
- Kutoa mchango kwa vyama vya ukombozi vya nchi za kusini mwa Afrika, kama; Zimbabwe {ZANU), Afrika Kusini (ANC na PAC), Namibia (SWAPO), Angola (MPLA) na Msumbiji (Frelimo)
CHANGAMOTO
Siasa zake za ujamaa zilishindwa baada ya mwaka 1976. Baada ya kuona kuwa uchumi wa Tanzania hautaweza kusimama kwa siasa za kijamaa, na yeye kutoweza kuvumilia kuendesha nchi kwa siasa ambazo yeye hakuwa muumini, Nyerere kwa maamuzi yake mwenyewe aliamua kustaafu nafasi ya urais. na kuruhusu kufanyika uchaguzi mwaka 1985, uchaguzi ambao ulimsimamisha Ali Hassan Mwinyi kuwa Rais, ambaye alitawala kwa siasa za uchumi wa soko huria.UKOSOAJI DHIDI YAKE
- Mwl.Nyerere analaumiwa kwa siasa zake za kiujamaa kuwa zilichelewesha maendeleo ya Uchumi wa Tanzania.
| Mwalimu Julius K Nyerere |
Pia kuna makundi ya waislamu wanaomtuhumu kwa kuendesha kwa siri vita dhidi ya uislamu na upendeleo wa elimu na madaraka kwa wakristo.
SIFA ZAKE
Pamoja na changamoto na matatizo;- mwalimu kamwe hawezi kusahaulika kwa juhudi zake za kujenga umoja na mshikamano kwa watanzania, ambao ndio msingi wa amani tunayojivunia sasa.
- Bado anakumbukwa na watanzania hasa wa hali ya chini kutokana na sera zake za kujali utu na ubinadamu.
- Pia ataendelea kukumbukwa barani Afrika, hasa kwa mchango wake mkubwa wakati wa harakati za kupigania uhuru katika nchi mbali mbali barani Afrika.
- Mwalimu ni mmoja wa viongozi wachache wanaokumbukwa kwa kutojilimbikizia mali pamoja na kutawala kwake miaka zaidi ya 24.
- Mwalimu ni mfano wa kuigwa kama kiongozi aliyefuata misingi ya maadili ya uongozi
na mzalendo wa nchi hii.
Mwishoni mwa maisha yake Mwalimu Nyerere aliishi kama mkulima wa kawaida kijijini kwake Butiama.
Tarehe 14 Oktoba, 1999 mauti yalimkuta, kutokana na ugonjwa wa saratani ya damu (Leukemia). Alizikwa sehemu alikozaliwa kijijini Butiama, mkoa wa Mara Mashariki mwa ziwa Victoria. Mwalimu aliacha mjane, watoto na wajukuu.
![]() |
| kaburi la Nyerere kijijini Butiama |
HAKIKA TUTAENDELEA KUMKUMBUKA HAYATI MWALIMU NYERERE.
MUNGU AILAZE ROHO YAKE MAHALI PEMA PEPONI.
AMINA.



